utt

.

line

line

line of success

line of success

Wednesday, June 17, 2015

Kibano cha wagombea urais CCM hiki hapa

Dar/Mikoani. Masharti yaliyomo katika fomu za wagombea urais za CCM huenda yakawa mtihani kwa baadhi yao, hasa katika kipengele kinachohoji iwapo mgombea aliwahi kujiunga na chama kingine cha siasa zaidi ya Tanu na Afro Shiraz Party (ASP).
Wagombea hao jana waliendelea kusaka wadhamini huku Makongoro Nyerere, akieleza kuwa kuna ugonjwa wa kuvunja kanuni na Stephen Wasira akisema hakuna mafisadi ndani ya CCM wakati Dk Gharib Mohamed Bilal na Samuel Sitta wakirejesha fomu.
Fomu hizo, ambazo wagombea 34 wamezijaza na wanatakiwa kuzipeleka mikoa mbalimbali kutafuta wadhamini, ndizo zitakazotumika kujadili makada hao na kuwachuja hadi kubakia wagombea wasiozidi watano ambao watapelekwa Halmashauri Kuu na baadaye Mkutano Mkuu kwa ajili ya kupigiwa kura kupata mwanachama atakayepeperusha bendera ya CCM.
Kwa mujibu wa fomu hizo ambazo Mwananchi imepata nakala zake, wagombea hao watatakiwa waeleze iwapo waliwahi kukihama chama hicho kikongwe au ASP, kutaja jina la chama walichojiunga nacho na kueleza walikaa huko kwa muda gani.
Wagombea watakaotakiwa kutoa maelezo kwenye kipengele hicho ni mwanasiasa mkongwe, Stephen Wasira na mbunge wa Afrika Mashariki, Makongoro Nyerere.
Makada hao wawili waliihama CCM wakati wa uchaguzi mkuu wa kwanza tangu kurejeshwa kwa siasa za vyama vingi nchini mwaka 1995, na kuhamia NCCR-Mageuzi na wote walishinda ubunge.
Hata hivyo, ubunge wa Makongoro ulitenguliwa na mahakama wakati Wasira alimaliza kipindi chake cha miaka mitano.
Hata hivyo, kigezo hicho ni sehemu tu ya maswali yaliyowekwa kwenye fomu hiyo na itategemea jinsi watakavyojieleza kukidhi Kamati Kuu ya CCM ambayo inaundwa na vigogo 34.
Vilevile fomu hizo zinawataka makada wanaoomba kuteuliwa kuwania nafasi hiyo ya juu nchini, kueleza iwapo waliwahi kuadhibiwa na chama au na jumuiya ya chama kwa kosa lolote.
Kipengele hiki kinaweza kuwabana wagombea sita waliopewa onyo kali na Kamati Kuu kwa kuanza kampeni mapema na kuhusiana na vitendo vinavyokiuka maadili.
Wagombea walioadhibiwa kwa kosa hilo ni Wasira na mawaziri wakuu wa zamani, Edward Lowassa na Frederick Sumaye. Wengine ni January Makamba, ambaye ni Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Taknolojia, William Ngeleja (mbunge wa Sengerema) na Bernard Membe (Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa).
Pia fomu hizo mbali na kuwataka wagombea kukusanya wadhamini 450 katika mikoa 15, mitatu kati yake ikiwa ya Zanzibar, zinamtaka kila mmoja kueleza iwapo aliwahi kupatikana na hatia mahakamani ya kukwepa kulipa kodi yoyote ya Serikali na kama aliwahi kufanya hivyo, ataje kodi gani na alipewa adhabu gani.

No comments:

Post a Comment