Dar/Mikoani. Waziri Mdogo wa Mambo ya Nje wa
Marekani anayeongoza Kitengo cha Masuala ya Afrika, Linda
Thomas-Greenfield amemuuliza Rais Jakaya Kikwete iwapo ana mtu wake
katika orodha ndefu ya makada waliojitokeza kuomba kuwania urais kwa
tiketi ya CCM.
Waziri huyo aliuliza swali hilo usiku wa kuamkia
Jumatatu (Juni 14, 2015) mjini Johannesburg, Afrika Kusini wakati
anazungumza na Rais Kikwete kutokana na wanachama wa CCM 35 kujitokeza
kuchukua fomu za kuwania urais.
Viongozi hao walikuwa wanahudhuria Mkutano wa 25
wa Umoja wa Afrika (AU) uliofanyika, kwa siku mbili, kwenye Kituo cha
Mikutano cha Sandton Convention jijini Johannesburg, Afrika Kusini na
kumalizika jana.
Makada hao wa CCM wameibua upinzani mkali kwenye
mbio za urais na hadi sasa hakuna dalili za mtu yeyote kuwa ana nafasi
kubwa ya kupitishwa, hali ambayo imesababisha vyombo vya habari
kubashiri kuwa mteule wa CCM anajulikana kwa viongozi wa juu wa chama
hicho tawala.
Wakati nchi ikijiandaa kupata kiongozi mpya
atakayeongoza Serikali ya Awamu ya Tano, mbio za urais ndani ya CCM
zimevutia idadi kubwa ya wanachama ambayo haijawahi kutokea kabla na
baada ya kurejeshwa kwa mfumo wa vyama vingi nchini mwaka 1992 baada ya
watu 35 kuchukua fomu hadi sasa.
Mwaka 1995, wanaCCM waliojitokeza kutaka kumrithi
Rais Ali Hassan Mwinyi walikuwa 15 na mwaka 2005 waliojitokeza kutaka
kumrithi Rais Benjamin Mkapa walikuwa 11.
Taarifa ya Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais, Ikulu
ilisema jana kuwa mwanzoni tu mwa mazungumzo baina ya viongozi hao,
Linda alimuuliza Rais Kikwete, “Je, unaye mgombea yeyote ambaye
unampendelea miongoni mwa utiriri wa wagombea”.
Baada ya swali hilo, kwa mujibu wa taarifa ya
Ikulu, Rais Kikwete alijibu, “Sina mgombea ninayempendelea. Wagombea
wote ni wa kwangu, ni wa chama changu, isipokuwa ninayo kura moja ambayo
kwa mujibu wa taratibu za haki katika chama chetu nitaitumia katika
vikao mbalimbali”.
Kuhusu utiriri wa wagombea, Rais Kikwete alisema wingi wa wagombea ni jambo zuri kwa CCM.
“Hiki ni chama kikubwa. Wingi unatupa nafasi ya
kujadili kwa nafasi nani awe mgombea wetu. Isitoshe, tunaona wagombea
wengi zamu hii kwa sababu ya wigo mkubwa wa uhuru ambao umejengeka
katika nchi yetu katika miaka ya karibuni.
“Vile vile, wingi wa wagombea unathibitisha
mafanikio yetu katika miaka 10 iliyopita kwa sababu tungeshindwa, watu
wangeogopa kujitokeza kugombea nafasi hiyo.”
Rais Kikwete alisema hana tatizo na wingi wa
wagombea kwa sababu haiwezekani kuwazuia watu kugombea nafasi hiyo kwa
sababu ni haki yao.
No comments:
Post a Comment